RAIS SAMIA DIRA YA WANAWAKE KATIKA MASUALA YA UONGOZI NA KIUCHUMI
Kuelekea Siku ya Wanawake Duniani
#KAZIINAONGEA
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ameimarisha vyema ushiriki wa wanawake katika uongozi na masuala ya kiuchumi nchini kwa kuwapa kipaumbele wanawake katika nafasi mbalimbali za uongozi sambamba na kujali maslahi yao.
Katika upande wa uongozi, wanawake walio wengi wameshika nafasi za juu akiwemo Waziri wa Ulinzi Dkt. Stergomera Tax, Waziri wa Utalii Balozi Dkt. Pindi Chana, Waziri wa Afya Jenista Mhagama, mbali na hilo, katika kujali maslahi ya wanawake Rais Samia ameimarisha afya ya mama sambamba na kutekeleza miradi mbalimbali ya wodi za wanawake, amekuwa kinara katika kampeni ya kupinga matumizi ya nishati chafu ili kuokoa afya na uhai wa wanawake Barani Afrika, Rais Samia pia ametoa mikopo yenye riba nafuu kwa wanawake.
Katika muktadha huo huo Serikali imeboresha mazingira ya wanawake nchini ili waweze kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za kiuchumi, maendeleo ya Tanzania na kushika nafasi za uongozi.
Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga amemshukuru Rais Samia katika kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo nchini yatafanyika mkoani Arusha,
"Kipekee namshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani amekuwa dira ya kutuongoza na kuhakikisha wanawake wengi zaidi tunashiriki katika shughuli za maendeleo na hata katika nafasi za uongozi." Amesema Kapinga
Amesema Rais Samia amekuwa kinara katika kuibua wanawake katika sekta mbalimbali za kiuchumi nchini.
Ameitaka jamii kuondokana na dhana kwamba mwanamke anapopewa nafasi ya uongozi anaweza kusahau majukumu yake mengine ya kijamii.
Aidha, Kapinga ametoa wito kwa wanawake kupendana, kushikamana, kusaidiana na kutembea kifua mbele katika kuelekea Siku ya Wanawake Duniani.
*#KAZIINAONGEA*
0 Comments